Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Kamanda Mohamed
Mpinga amesema mabadiliko ya sheria ya usalama barabarani hayaepukiki
ili kupunguza vifo na majeruhi vitokanavyo na ajali za barabarani.
Kamanda Mpinga amayesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa
Uzinduzi wa Programu ya Usalama Barabarani inayoratibiwa na Chama
cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA) kwa kushirikiana na wadau
mbali mbali wa Usalama Barabarani.
“Sheria zinazohusu masuala ya Usalama barabarani inabidi zifanyiwe
marekebisho ili ziweze kusaidia kupunguza vifo na majeruhi kwani zilivyo
sasa hazitoi adhabu kali kwa wanaokiuka sheria hizo”alisema Kamanda
Mpinga.
Aidha Kamanda huyo alisisitiza kuwa suala la Usalama Barabarani ni la
kila mmoja hivyo inabidi litiwe mkazo na watu wote.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa TAWLA, Bi Tike Mwambipile amesema
chama hicho kwa kuzingatia umuhimu wa kushughulikia masuala ya
Usalama Barabarani kimeona ni vyema kikafanya kikao hicho ili kupata
mawazo ya wadau.
Bi Mwambipile amesema vifo vingi vinavyotokana na ajali za barabarani
vinawaacha wanawake wengi wakiwa wajane na watoto yatima
wanaongezeka.
Ameongeza kuwa fedha nyingi zinatumika kuwahudumia majeruhi badala
ya kufanya shughuli nyingine za maendeleo ya jamii.
Naye Mwenyekiti wa TAWLA, Bi Aisha Bade amesema mabadiliko
makubwa ya sera na sheria za usalama barabarani ni lazima yafanyike ili
kupunguza athari zitokanazo na ajali za barabarani.
Bi Bade amesema TAWLA kwa kushirikiana na wadau wengine inafanya
juhudi za makusudi ili kuhakikisha sheria hizi zinabadilishwa ili
kukabiliana na janga hili.
Visababishi vya ajali kwa hapa nchini vimetajwa na Mratibu wa Mradi
Bloomberg wa Usalama Barabarani, Bi Mary Kessy kuwa ni ulevi,
kutofunga mkanda, kutoweka vizuizi vya watoto kwenye magari, mwendo
kasi na kutovaa kofia ngumu kwa waendesha pikipiki.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...